Serikali imesema itasambaza mabomba ya gesi nchi nzima ikibidi hadi nje ya nchi na kuiuza ili kujenga uchumi imara huku ikiahidi kuandaa mpango mkakati utakaowashirikisha wadau wakiwemo Ewura kuhakikisha bei ya umeme wa gesi inashuka ili watanzania wote waweze kunufaika na huduma hiyo.

Hayo yamesemwa na waziri wa nishati na madini Mh, George Simbachawene alipotembelea kituo cha uzalishaji wa umeme Ubungo namba mbili jijini Dar es Salaam kuona mitambo ya kuzalisha umeme wa gesi iliyowashwa na shirika la umeme nchini Tanesco ambapo tayari megawati 90 zimekwishaingia kwenye gridi ya taifa.
 
Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa shirika la umeme nchini Tanesco injinia Felshesm Mramba amesema mitambo iliyowashwa inazalisha umeme wa gesi kutoka Mtwara vizuri na hakuna hitilafu, mushkeri, wala dosari yeyote.
 
Uwekezaji wa mradi wa umeme wa gesi kutoka Mtwara kuja Kinyerezi hadi katika mitambo ya Ubungo jijini Dar es Salaam ni mkubwa kuliko yote nchini umegharimu kiasi cha  dola bilioni 1.22 na utamaliza tatizo la mgawo wa umeme nchini sambamba na kupunguza gharama kubwa kwa Tanesco kuzalisha umeme kwa kutumia vyanzo vya maji, mafuta mazito na mepesi ambapo kwa mujibu wa serikali licha ya kuwa na mpango mkubwa wa kujenga megawati 600 kwa mikoa ya kusini Lindi na Mtwara kwa kuanzia  imesema kitaalamu itapeleka megawati 20 ndani ya miezi miwili ili kumaliza kabisa tatizo la umeme kwenye mikoa hiyo kunakotokea gesi hiyo.

Post a Comment