Mwalimu wa Shule ya Sekondari Manushi Kibosho, Wilaya ya Moshi Vijijini ameuawa saa chache baada ya ugomvi unaohusishwa na kuchanwa kwa picha ya mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa.

Mwalimu huyo, Demetus Dastan (33) maarufu kwa jina la Kidule, aliuawa Jumamosi iliyopita usiku na mwili wake kukutwa katika shamba la mtu aliyetajwa kuwa ni Joackim Massawe.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Fulgence Ngonyani alisema kabla ya kuuawa, mwalimu huyo alikuwa amekwenda kunywa pombe katika klabu moja hapo kijijini. Inadaiwa kuwa akiwa klabuni, kulitokea ubishani kati yake na mtu mwingine uliotokana na kuchanwa kwa picha ya Lowassa ambao ulikwenda mbali na kusababisha wapigane.

Kamanda Ngonyani alisema waliamuliwa na wateja wengine waliokuwapo na baadaye mwalimu huyo aliondoka kurejea nyumbani na hakuonekana hadi mwili wake ulipookotwa.

Baadaye mwili wake ulikutwa shambani ukiwa na michubuko kidogo kwenye mguu wa kulia karibu na goti na shati lake likiwa limechanikachanika.

Polisi wamewakamata watu wawili akiwamo mmiliki wa klabu hiyo na mtu mwingine anayedaiwa kuwa aliongozana naye kurudi nyumbani huku mtu waliyepigana naye akiendelea kusakwa.

Post a Comment