Makamu wa rais Dk Mohamed Gharib Bilal amewaongoza waombolezaji kuuaga mwili wa aliyekuwa waziri wa nchi, ofisi ya rais, menejimenti ya utumishi wa umma Mh Celine Kombani zoezi lililofanyika viwanja vya Kareemje jijini Dar es Salaam kabla ya kusafirishwa kwenda mkoani Morogoro kwa maziko.


Mara baada ya mwili huo kuwasili katika viwanja hivyo mchungaji Wilfred Mmari ameongoza ibada fupi ya kumuombea marehemu kabla ya makundi mbalimbali kutoa salaam zao za rambirambi.
 
Akisoma salamu za serikali waziri wa nchi ofisi ya waziri mkuu sera, uratibu na bunge Mh Jenista Mhagama mbali na kueleza uadilifu uliotukuka wa marehemu Kombani amesema ndani ya serikali ameacha pengo huku mwakilishi wa serikali ya mapinduzi Zanzibar naye akitoa salaam.
 
Naye spika wa bunge anayemaliza muda wake Mh Anne Makinda akitoa salaam kwa niaba ya ofisi ya bunge amewataka watumishi wa umma kutumia msiba huo kutafakari na kurekebisha maisha yao kwa kuwa na upendo na kuwatumikia wananchi kwa kutoa huduma bora.
 
Baadhi ya mawaziri wenzake na wabunge waliojitokeza kuuaga mwili huo wamemwelezea marehemu Kombani namna alivyokuwa mwalimu wao kila mara walipotaka ushauri wake ndani na nje ya bunge.
 
Mbali na makamu wa rais baadhi ya viongozi wengine waliohudhuria zoezi hilo ni pamoja na mawaziri, wabunge, viongozi wa vyama vya siasa, mama Maria Nyerere na mama Salma Kikwete.
 
Akisoma wasifu wa marehemu mwakilishi wa serikali amesema marehemu alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa saratani ya kongosho iliyokuwa imeathiri ini lake na alizaliwa june 19 1959 na kufarifariki dunia septemba 24 mwaka huu katika hospitali ya Apollo nchini India na mwili wake unatarajiwa kuzikwa sept 29 mkoani Morogoro na ameacha mume,watoto watano na wajukuu wanne.
 

Post a Comment