Viongozi wa dini, taasisi zisizokuwa za kiserikali na vyama vya siasa vimelitaka jeshi la polisi na tume za taifa za uchaguzi NEC na ZEC kutenda haki na kuwa wawazi kwa kila jambo ambalo wananchi na wadau wanapaswa kujua ili amani iendelee kudumu wakati wa uchaguzi na hata baada ya uchaguzi.
Wakizungumza katika kongamano la amani na utulivu wakati wa uchaguzi mkuu lililoshirikisha wadau mbalimbali, na kufanyika jijini Dar es Salaam baadhi ya viongozi wa dini walioshiriki wamesema amani ni tunda la haki hivyo kila mmoja akitimiza wajibu wake ipasavyo kwa kutenda haki na kuzingatia sheria uchaguzi mkuu utamalizika kwa amani na utulivu.
 
Baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa nao wakaelezea mambo kadhaa yanayochangia uvunjifu wa amani hasa wakati wa uchaguzi huku wengine wakiahidi kuendelea kuonyesha ustahamilivu na ustaarabu wakati wote wa kampeni ikiwa ni pamoja na kutii sheria bila shuruti na kuvitahadharisha vyombo vinavyosimamia uchaguzi kutokuhubiri suala la amani midomoni tu badala yake waonyeshe kwa vitendo kwa kusimamia haki.
 
Mwenyekiti wa baraza la vyama vya siasa Peter Mzirai amesema mijadala ya mara kwa mara kuelekea uchaguzi mkuu ndio kiungo muhimu na kushauri kuundwa kwa kamati ya kupokea migogoro ya vyama vya siasa na ishughulikiwe kwa wakati huku mkuu wa operesheni na mafunzo wa jeshi la polisi Paul Chagonja akijibu hoja kadhaa na kuwataka wanasiasa kueleza sera zao wawapo majukwaani badala ya kuanza kukashfiana.
 
Akihitimisha kongamano hilo mwakilishi kutoka tume ya uchaguzi Zanzibar ZEC pamoja na kujibu hoja zilizohusu NEC Bw Ramadhan Omary Mapuri amesema suala la wanafunzi wa vyuo vikuu watumie fursa ya kuhakiki majina kwa kwenda kwenye halmashauri au vituo walivyojiandikishia kubadilisha taarifa zao huku mwakilishi wa MOAT Bw Henry Muhanika akielezea hatua walizochukuwa katika kutoa elimu kwa wanahabari.
 

Post a Comment