Siku moja baada ya kutangaza kujitoa CCM, kada mkongwe wa chama hicho, Balozi Juma Mwapachu amesema uamuzi alioufanya ni sahihi ambao hata Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere angekuwa hai angeufanya kwa sasa.

Balozi Mwapachu alieleza hayo jana katika mahojiano maalumu na kuongeza kuwa chama chake cha zamani kimepoteza mwelekeo kwa kuwa kinara wa kuvunja katiba na taratibu kitendo ambacho Nyerere alikichukia katika maisha yake.

Alisema anafahamu fika kuna watu watakosoa uamuzi wake huo lakini hatababaishwa na maneno yao na atasimamia msimamo wake huo huku akieleza kuwa anajisikia amani kujitoa katika siku ya kumbukumbu ya miaka 16 ya kifo cha Nyerere.

Mwapachu alitangaza kujitoa CCM juzi akisema kilivunja taratibu wakati wa mchakato wa uteuzi wa mgombea wa urais uliofanyika Julai ambao Dk John Magufuli alichaguliwa.

“Nimefanya makusudi kujitoa wakati huu kwa sababu hata Nyerere mwenye angekuwapo hai leo hii angefanya uamuzi kama niliofanya. Hata yeye alikuwa ameshachoshwa na chama chake kwa uvunjaji wa kanuni, taratibu na katiba na alikwishaona kuwa kinaanza kupitwa na wakati.” 
 
Alisema mengine yanayojitokeza kwa sasa ndani ya CCM yanaonyesha bayana kuwa chama hicho hakiendi na wakati na kilijisahau na kuendesha mambo kama kipo kwenye mfumo wa chama kimoja wakati ni wa vyama vingi.

Alisema CCM ya sasa siyo ile aliyojiunga nayo akiwa chuo kikuu, ndiyo maana amejitoa kutokana na kutekwa na watu wachache ambao humpiga vita mtu ambaye si mwenzao.

Post a Comment