Wakati waswahili wanasema adui yako mwombee njaa, msemo huo
umekuwa tofauti kwa upande wa mgombea ubunge wa ACT – Wazalendo Jimbo la
Arusha Mjini, Estomih Malla baada ya jana kupanda jukwaani na kumwombea
kura za ndiyo mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa.
Mgombea huyo alikuwa akihutubia mkutano wa kampeni uliokuwa na
lengo la kunadi pia sera na kumwombea kura mgombea wa chama chake, Anna
Mnghwira, katika Uwanja wa Stendi Kubwa, mkoani hapa.
“Jamani naombeni mtambue kuwa mimi ni msomi ambaye nina shahada
(Hakuitaja ni ya nini), kwa muda mrefu sasa nimekuwa nikitumia elimu
yangu kwa faida ya familia yangu tu baada ya kufukuzwa udiwani na
Chadema, sasa naombeni mnichague ili niitumie pia kuwatumikia kwa
kuwaletea maendeleo yaliyoshindikana kupatikana kwa miaka mitano,” alisema.
Mgombea huyo, alisema maendeleo ya kweli yanaletwa na watu wa kweli na wazalendo. “Mimi
ni mkweli, nipeni ridhaa ya kuwaongoza na msisahau kumpa ridhaa ya kuwa
rais mheshimiwa Edward Lowassa, naamini hamtajutia kura zenu,” alisema Malla.
Alipoulizwa baada ya kumaliza mkutano wake kwa nini amemnadi
Lowassa badala ya mgombea urais wa chama chake, Malla hakutaka kujibu
bali alipanda gari lake na kuondoka.
Post a Comment