Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimemteua kada wake, Christopher Ole Sendeka, kuwa msemaji wa chama hicho akichukua nafasi ya Nape Nnauye, ambaye kwa sasa ni Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo.
 
Akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu ya CCM Lumumba jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana, alisema Nape ataendelea kuwa na wadhifa wa Katibu wa Itikadi na Uenezi, lakini shughuli za usemaji wa chama zitafanywa na Sendeka.
 
“Kwa taratibu zetu, Mtendaji wa Chama anapoteuliwa kwenye majukumu mengine, anatakiwa kuachia ngazi. Hivyo tumemchagua Ole Sendeka kuwa Msemaji. Uteuzi wa Nape uko katika Halmashauri Kuu, hivyo utenguzi wake utasubiri vikao hivyo vitakavyokaa hivi karibuni,” alisema.
 
Katika hatua nyingine, Kinana alisisitiza kuwa Mwenyekiti wa chama hicho, Jakaya Kikwete, atakabidhi kijiti cha uongozi kwa Dk. John Magufuli, Juni, mwaka huu baada ya kuridhia kubeba majukumu hayo.
Kwa upande wake, Sendeka alimpongeza Rais Magufuli kwa kutekeleza kwa vitendo kauli ya Hapa Kazi tu, na kwamba umejidhihirisha katika kipindi kifupi cha uongozi kwa kudhibiti rushwa, ufisadi na ubadhirifu wa mali za umma, matumizi mabaya ya madaraka na ukwepaji kodi na matokeo yake yanaoonekana.
 
“…matokeo hayo ni pamoja na kuongezeka kwa makusanyo ya kodi ya serikali ambayo yameiongezea uwezo wa kuwahudumia wananchi kujikwamua na umaskini kwa ustawi wa jamii kwa ujumla,” alisema.
 
Aidha, alisema CCM inamuunga mkono Rais Magufuli kwa hatua zozote anazozichukua katika kurudisha nidhamu na uwajibikaji katika utumishi wa umma na kwa walioguswa kwa namna moja au nyingine, wamefanyiwa kwa kuzingatia sheria na misingi ya utawala bora.
 
Kuhusu kupokea wanachama waliokihama chama hicho na kurudi, Kinana alisema wataweka utaratibu wa kuwachuja wale ambao waliondoka bila kutoa lugha za matusi, kejeli na kashfa nyingine na maslahi binafsi, kwa waliotenda hayo watafikiriwa na kwamba maoni ya wanachama yamepokelewa na yatafanyiwa kazi.

Post a Comment