Waziri Mkuu Mstaafu wa awamu ya Nne Mhe. Mizengo Pinda ametoa wito kwa watumishi wa Umma kufanya kazi kwa bidii na kuzingatia sheria na taratibu ili kuendana na kasi ya serikali ya awamu ya tano ya kuwahudimia wananchi na kukabiliana na umasikini.

Akizungumza wakati akifunga mkutano wa kikao cha ushauri cha mkoa wa Katavi(RCC), Pinda  amezishauri halmashauri kufuata taratibu za manunuzi na matumizi ya pesa kwa maslahi ya Umma ili kupiga hatua katika maendeleo ya mwananchi mmoja mmoja.

Mhe. Pinda amesema licha ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi wa umma katika utendaji wao ila amewataka watanzania kujenga tabia ya kutokukubali kuwajibishwa kutokana na ukiukwaji wa utumishi wa Umma.

Aidha waziri Mkuu huyo Mstaafu amewataka viongozi na Wananchi wa Mkoa wa Katavi kuumunga mkono na kumuombea rais Magufuli katika jitihada zake za kupambana na ufisadi ili kuleta maendeleo ambayo yalihodhiwa na watu wachache.

Mhe. Pinda ameongeza kuwa kwa mwendo wa Rais Magufuli anaamini kuwa ndani ya kipindi chake cha miaka kumi kama akifanikiwa kumaliza vipindi vyote basi kutokana na kasi yake Tanzania itakua imepiga hatua kubwa za kiuchumi na kuwa ni moja kati ya nchi zenye uchumi wa kati.

Post a Comment